Tarehe 05 May 2026 Mheshimiwa Meja Jenerali Richard Mutayoba Makanzo aliwasilisha Hati za Utambulisho kwa Mheshimiwa Jenerali Joseph Aoun, Rais wa Jamhuri ya Lebanon, katika Ikulu ya nchi hiyo jijini Beirut.
Katika mazungumzo yake alitoa shukurani kwa Mheshimiwa Rais na Seikali ya Lebanon kwa kumpatia fursa hiyo adhimu. Aidha, Mheshimiwa Balozi alitoa salamu za Mheshimiwa Dk. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa Mheshimiwa Aoun, na pole kwa wananchi wa Lebanon waliopoteza maisha, mali na ambao wamehama makaazi yao kutokana na vita vinavyoendelea, katika eneo la Kusini la nchi hiyo.
Mheshimiwa Balozi pia alimuhakikishia Mheshimiwa Joseph Aoun kuwa Tanzania iko pamoja na Lebanon bega kwa bega muda wote kupitia sala, na ushirikiano wetu katika Ulinzi wa Amani nchini humo, ambapo JWTZ ni miongoni mwa Majeshi yanayounda Kikundi cha UNIFIL.
Mwisho, alimuhakikishia Mheshimiwa Rais juu ya utayari wake katika kuunganisha watu wa mataifa hayo mawili kupitia ushirikiano wa kidplomasia, biashara na uwekezaji. Alisisitiza kuwa lango kuu la Bandari ya Dar es Salaam linaweza kutumika kupanua wigo wa biashara linalounganisha soko la EAC na SADC.
Mheshimiwa Balozi alimalizia kwa kueleza kuwa Tanzania ina utulivu na amani utakayowezesha wafanyabiashara wa pande zote kutumia maliasili zilizopo kukuza ushirikiano, biashara na uwekezaji.
Kwa upande wake Mheshimiwa Rais alitoa shukurani kwa Serikali ya Tanzania na kutoa Salam zake kwa Mheshimiwa Rais Dk. Samia Suluhu Hassan na kupongeza kwa utulivu na amani iliyopo nchini Tanzania.
Aidha, aliwasilisha ombi la kuwa na Ubalozi nchini Lebanon. Mwisho alitoa shukurani kwa Serikali ya Tanzania kwa kwa uamuzi wake wa kuwa miongoni mwa nchi za zinazounda UNIFIL. Awali, kabla ya kukutana Mheshimiwa Rais, Mheshimiwa Balozi alikutana na Waziri wa Mambo ya Nje wa nchi hiyo na kukabidhi Kivuli cha Hati za Utambulisho.





